Katika hafla ya utoaji wa tuzo kwa walimu waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, iliyofanyika Mei 30, 2025 katika uwanja wa Nyamagana, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mhe. Amina Nassoro Makilagi, alisisitiza kuwa mafanikio ya sekta ya elimu hayawezi kuletwa na kundi moja pekee. Alitoa wito kwa jamii nzima, hususan wazazi, kushirikiana na walimu katika kuimarisha mazingira ya kujifunzia.
"Mafanikio ya sekta ya elimu hayawezi kuletwa kwa kundi moja hivyo niwatake wazazi kushirikiana na walimu kuendeleza baadhi ya miundombinu ambayo wanakuwa wamekubaliana katika vikao, ili elimu bora iweze kupatikana kwa wanafunzi," alisema Mhe. Makilagi.
Aidha, aliwahimiza walimu kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwani kupitia juhudi zao, taifa hupata wataalamu mbalimbali kama madaktari, wanajeshi, marubani na wengine wengi.
"Walimu endeleeni kupiga kazi maana kupitia nyie tunawapata watu wa kada tofauti. Walimu oyeee!" alisisitiza kwa shangwe"
Mhe. Makilagi aliwapongeza viongozi wa shule na walimu kwa jitihada zao, hususan Afisa Elimu wa Wilaya, Mhe. Ally Mussa Rambwe, kwa mchango wake mkubwa katika kuhakikisha ufaulu wa wanafunzi unabaki juu.
Kwa mwaka 2024, ufaulu wa wanafunzi wa darasa la saba umefikia asilimia 93%, hali inayoifanya Nyamagana kushika nafasi ya pili kimkoa. Alitoa wito wa kurejesha nafasi ya kwanza kupitia mshikamano na juhudi zaidi.
Mthibiti Ubora wa Shule Wilaya ya Nyamagana, Mhe. Lucy Nyanda, alimpongeza Afisa Elimu kwa kuratibu tukio hilo muhimu la kuwajumuisha walimu na kuongeza mshikamano. Alipendekeza mikutano kama hiyo ifanyike mara kwa mara, hata kila mwisho wa mwezi.
Kwa upande wao, wawakilishi wa Benki ya NMB walieleza namna taasisi yao imekuwa bega kwa bega na walimu kwa miaka mingi, wakiahidi kuendeleza ushirikiano katika nyanja za kifedha na kitaaluma.
Shughuli hiyo pia ilihusisha michezo mbalimbali kwa ajili ya burudani na kujenga afya za walimu, ikiwemo kukimbiza kuku, mpira wa miguu, kuvuta kamba, na mbio za magunia. Tuzo zilitolewa kwa walimu na shule zilizofanya vizuri.
Kwa shule za serikali, waliotajwa ni Butimba A, Butimba B, Sahara, na Buhongwa; huku shule za binafsi zilizoibuka ni Buyegu, Mzigu, na Rehoboth.
Hafla hii imedhihirisha kuwa mshikamano baina ya walimu, viongozi, wazazi na wadau wengine ni chachu ya mafanikio ya elimu. Kwa pamoja, ndoto ya elimu bora na mazingira rafiki ya kujifunzia inawezekana.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.