Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda, amefungua rasmi mafunzo ya awamu ya kwanza kwa Waheshimiwa Madiwani waliochaguliwa katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 kutoka Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Manispaa ya Ilemela, pamoja na Halmashauri za Wilaya za Magu na Ukerewe.
Akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi, Mhe. Mtanda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwapatia madiwani maarifa na stadi muhimu zitakazowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hususan katika maeneo ya uongozi na utawala bora, sheria na taratibu za Serikali za Mitaa, pamoja na uendeshaji sahihi wa vikao na mikutano ya kisheria.
Ameeleza kuwa mafunzo hayo pia yamejumuisha masuala ya uandaaji wa mipango na bajeti, usimamizi wa watumishi, pamoja na ufuatiliaji na usimamizi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao.
Mhe. Mtanda amebainisha kuwa bado kumeendelea kuwepo kwa uelewa usio sahihi kuhusu wajibu wa usimamizi wa miradi ya maendeleo, ambapo baadhi ya viongozi na wananchi wamekuwa wakiamini jukumu hilo limekuwa la Wakuu wa Mikoa au Wilaya pekee, hali iliyosababisha baadhi ya madiwani kujiona kuwa si wajibu wao kusimamia utekelezaji wa miradi.
Ameweka bayana kuwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo ya madiwani umekuwa ni msingi wa uaminifu waliokabidhiwa na wananchi, na amewahimiza madiwani kusimamia miradi hiyo kwa karibu, kubaini changamoto mapema, kutoa taarifa pale dosari zinapobainika, na kuhakikisha rasilimali za umma zimetumika kwa malengo yaliyokusudiwa.
Aidha, ametoa maelekezo kwa wakufunzi kuhakikisha kuwa mada zinazohusu mahusiano ya kiutendaji kati ya Halmashauri na Sekretarieti za Mikoa zimeelezwa kwa kina, sambamba na kufafanua mipaka ya majukumu kati ya madiwani na watendaji wa serikali katika ngazi ya kata, ili kuepusha migongano na kuimarisha mshikamano katika utekelezaji wa majukumu.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI amesema kuwa mafunzo hayo yamepangwa kutolewa kwa muda wa siku tatu na yamehusisha mada 11, zikiwemo uongozi na utawala bora, muundo na madaraka ya Serikali za Mitaa, pamoja na taratibu za uendeshaji wa vikao na mikutano ya kisheria.
Ameongeza kuwa mada zinazohusu mipango, bajeti, usimamizi wa miradi na udhibiti wa fedha zimeandaliwa kwa lengo la kuwajengea madiwani uwezo wa kusimamia rasilimali za umma kwa uwajibikaji na ufanisi.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mtanda ametoa maelekezo kwa Halmashauri ambazo bado hazijafikia kiwango cha matumizi cha asilimia 80 ya mashine za POS, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, kuhakikisha zimekamilisha ununuzi wa mashine hizo ndani ya kipindi cha miezi mitatu na zimewasilisha taarifa ya utekelezaji katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.