Katibu Tawala wa Wilaya ya Nyamagana, Thomas Salala, amewataka wadau wa biashara pamoja na taasisi mbalimbali za serikali kuendelea kushirikiana ili kukuza uchumi wa eneo hilo na wa Mwanza kwa ujumla.
Akizungumza leo katika kikao cha Baraza la Biashara Ngazi ya Wilaya ya Nyamagana kilichofanyika katika Ukumbi Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Katibu Tawala huyo aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi, alisema ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi za serikali ni msingi muhimu wa maendeleo ya uchumi wa halmashauri.
Alisisitiza kuwa uchumi ni mhimili mkuu wa maendeleo, hivyo wadau wanapaswa kuendelea kushirikiana ili kuhakikisha ukuaji wa uchumi unaendelea kuimarika siku hadi siku.
Kikao cha Baraza la Biashara ngazi ya wilaya hufanyika kila mwaka kwa lengo la kupitia ajenda mbalimbali za maendeleo ya kiuchumi ikiwemo taarifa ya usafirishaji wa mizigo na fursa zitokanazo na uwepo wa Bandari Kavu katika mradi wa SGR Misungwi, utoaji wa elimu ya Bima kwa Wote, utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu pamoja na uwepo wa fursa mbalimbali za uwekezaji ndani ya jiji.
Aidha katika kikao hicho wajumbe walijadili utekelezaji wa ajenda za mwaka 2022/2023 zikiwemo jitihada za utoaji wa elimu ya ushuru wa huduma kwa wafanyabiashara inayofanywa na Maafisa Biashara wa halmashauri kwa kushirikiana na TRA ambapo elimu hiyo inaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali ya biashara ikiwemo Soko Kuu kwa lengo la kuongeza uelewa na ufuasi wa sheria za kodi kwa wafanyabiashara.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.