Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda, amepongeza juhudi zinazoendelea kufanywa na Halmashauri ya Jiji la Mwanza katika kupunguza kwa kiwango kikubwa changamoto ya upungufu wa madawati katika shule za elimu ya awali na msingi.
Pongezi hizo amezitoa wakati wa hafla ya kukabidhi madawati 2,939 kwa shule 13 zilizopo ndani ya Jiji la Mwanza. Madawati hayo yametengenezwa kwa gharama ya Shilingi 440,800,000 ikiwa ni sehemu ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango wa kuimarisha miundombinu ya elimu.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mtanda amesema Mkoa wa Mwanza bado unakabiliwa na upungufu wa madawati 61,808, huku Jiji la Mwanza likiwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika zaidi. Hata hivyo, amepongeza hatua ya uongozi wa Jiji kuanzisha mkakati mahsusi wa kukabiliana na hali hiyo.
Ameeleza kuwa kukamilika kwa awamu ya kwanza kutapunguza kwa kiasi kikubwa uhaba huo na kubakiza takribani madawati 2,000 pekee, ambayo yamepangwa kushughulikiwa ndani ya mwaka huu wa fedha.
“Ninawapongeza kwa kasi hii ya utekelezaji. Ni wajibu wa kila halmashauri kuhakikisha mwanafunzi anapata mazingira bora ya kujifunzia,” amesisitiza.
Aidha, Mkuu wa Mkoa amezitaka halmashauri zenye changamoto kubwa ya madawati, ikiwemo Jiji la Mwanza, Kwimba, Magu na Sengerema, kuanzisha karakana za kutengeneza madawati ili kupunguza gharama na kuongeza uzalishaji.
Ameongeza kuwa ofisi yake itafanya ufuatiliaji wa karibu ndani ya miezi mitatu ijayo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Wakili Kiomoni Kibamba, amesema lengo lao ni kuhakikisha hakuna mwanafunzi anayekaa chini darasani.
Amebainisha kuwa mgawanyo wa madawati umezingatia mahitaji halisi ya kila shule, na kwamba ifikapo Juni mwaka huu kila darasa litakuwa na wastani wa madawati 30 ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.