Katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayotarajiwa kufanyika kitaifa tarehe 5 Juni 2025 jijini Dodoma, Wilaya ya Nyamagana leo imefanya zoezi kubwa la usafi wa mazingira katika kata ya Buhongwa, likiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mhe. Amina Makilagi, akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Akizungumza baada ya zoezi hilo, Mhe. Makilagi alisema kuwa usafi huo umefanyika kwa pamoja na kata zote za Wilaya ya Nyamagana chini ya usimamizi wa watendaji wa kata na Madiwani na kuongeza kuwa Tanzania inaungana na mataifa yote duniani kuadhimisha siku hii muhimu kwa kutekeleza kaulimbiu ya mwaka huu: "Tanzania Ijayo Tuwajibike Sasa, Dhibiti Matumizi ya Plastiki."
Mhe. Makilagi pia alieleza kuwa Nyamagana ilipangiwa kupanda miti milioni 1.5, na hadi sasa wilaya imevuka lengo hilo hatua inayosaidia kupunguza hewa ukaa na kuchochea mvua.
Aidha, alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi tarehe 19 Juni 2025 kumpokea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, atakapozindua rasmi mradi mkubwa wa maji kutoka Butimba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 46.
Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Jiji la Mwanza, Bw. David Joseph, alisema kuwa Siku ya Mazingira huambatana na kampeni za usafi, upandaji miti, na utoaji wa elimu ya mazingira. “Leo tumeungana na wananchi wa Buhongwa kufanya usafi na kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira kwa vitendo,” alisema.
Vijana nao hawakubaki nyuma. Muajabu Salum, mwanafunzi kutoka Shule ya Sekondari Nyaburogoya, kupitia klabu ya mazingira ya shule yao, alieleza kuwa wanaendeleza kampeni ya: “Linda Mazingira, Okoa Maisha”, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Utunzaji wa Mazingira 2022–2032 unaosimamiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
Mwisho, Mhe. Makilagi aliwahimiza wananchi kutumia haki yao ya msingi ya kupiga kura kwa mujibu wa Katiba ya mwaka 1977, na kupuuza kauli potofu zinazodhoofisha ushiriki wa kiraia katika maendeleo ya Taifa.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.