Watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza wameshiriki mafunzo ya matumizi ya mfumo wa kidijitali wa utunzaji na uendeshaji wa kumbukumbu na nyaraka za Serikali (e-Office), yaliyofanyika leo Oktoba 1, 2025 katika Ukumbi Mkubwa wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza.
Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo watumishi katika matumizi sahihi ya mfumo wa e-Office kama sehemu ya utekelezaji wa sera na miongozo ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu mageuzi ya TEHAMA katika utendaji kazi wa taasisi za umma.
Akitoa mafunzo hayo, Bw. Ally A. Ally, Afisa TEHAMA kutoka Ofisi ya Rais – Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Serikali, amewahimiza watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza kuutumia kikamilifu mfumo wa e-Office katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku, akisisitiza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mifumo ya kidijitali kwa lengo la kuongeza ufanisi, uwajibikaji na uwazi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.
Bw. Ally amesema kuwa matumizi ya mfumo wa e-Office ni sehemu ya mabadiliko makubwa ya kiutendaji yanayoendana na wakati wa sasa, ambapo Serikali inalenga kuachana na matumizi makubwa ya nyaraka za karatasi na badala yake kutumia mifumo ya kisasa inayorahisisha uhifadhi, ufuatiliaji na upatikanaji wa taarifa kwa haraka na kwa usalama zaidi.
Ameeleza kuwa lengo kuu la mfumo wa e-Office ni kurahisisha utendaji kazi, kuboresha mawasiliano ya kikazi, na kuimarisha usalama wa nyaraka za Serikali, sambamba na kuhakikisha kila mtumishi anatekeleza majukumu yake kwa wakati, kwa ufanisi na kwa kuzingatia taratibu na sheria zilizopo.
Aidha, amefafanua kuwa mfumo wa e-Office humtaka kila mtumishi kuwajibika moja kwa moja katika majukumu aliyopewa, kwa kuwa kila hatua ya utekelezaji wa kazi hurekodiwa ndani ya mfumo, hivyo kusaidia katika ufuatiliaji, tathmini ya utendaji kazi na uwajibikaji wa watumishi.
Kwa upande wao, watumishi walioshiriki mafunzo hayo wameonesha kuridhishwa na mafunzo yaliyotolewa, wakibainisha kuwa yamewasaidia kuongeza uelewa kuhusu matumizi ya mfumo wa e-Office na umuhimu wake katika kuboresha utendaji kazi wa kila siku ndani ya Halmashauri.
Halmashauri ya Jiji la Mwanza itaendelea kushirikiana na Ofisi ya Rais – Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Serikali katika kuhakikisha mifumo ya kidijitali inatumika ipasavyo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha utawala bora, kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.