Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mhe. Dkt. Festo John Dugange, amefungua rasmi Mkutano Mkuu wa 25 wa Jumuiya ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Kanda ya Ziwa Victoria (LVRLAC) uliofanyika Mei 26, 2025 katika ukumbi wa Kwatunza Beach Resort, Ilemela. Alimwakilisha Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Mashaka Biteko, aliyetoa salamu kwa wajumbe na kueleza kutoweza kuhudhuria kutokana na majukumu mengine ya kitaifa.
Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi wa Serikali, wajumbe wa LVRLAC, wadau wa maendeleo, na wageni waalikwa, ukiwa na kaulimbiu: “Shiriki Uchaguzi Mkuu 2025, Chagua Viongozi Bora.”
Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mhe. Dkt. Dugange aliipongeza LVRLAC kwa kuendelea kushirikiana na wadau kama benki ya NMB katika kuandaa mikutano yenye ajenda za maendeleo kwa wakazi wa Ukanda wa Ziwa Victoria. Aliahidi kuwa Serikali kupitia TAMISEMI itaendelea kutoa ushirikiano kuhakikisha rasilimali za Ziwa Victoria zinalindwa na kuendelezwa kwa manufaa ya wananchi.
Pia Mhe. Dkt. Dugange alizihimiza Halmashauri wanachama wa LVRLAC kupitia Mameya/ Wenyeviti na Wakurugenzi kusimamia ipasavyo ukusanyaji wa mapato ya ndani ili ziweze kujitegemea kwa zaidi ya asilimia 80.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Ndugu Fulgence S. Matemele alisisitiza umoja miongoni mwa Halmashauri wanachama na kuwaagiza Wakurugenzi kuhakikisha wanatenga fedha kwa ajili ya malipo ya ada ya mwaka na kuahidi kushirikiana na uongozi wa LVRLAC katika kuhakikisha kila Halmashauri inalipa michango kwa wakati.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa LVRLAC, Mhe. Willium Gumbo, alisema kwa zaidi ya miaka 20, jumuiya hiyo imekuwa ikijenga uwezo wa Serikali za Mitaa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kukuza maendeleo na ustawi wa jamii.
Katibu Mkuu wa LVRLAC, Bw. Billy Albert Brown, alieleza kuwa mkutano huo umeimarisha mshikamano na ushirikiano baina ya Halmashauri wanachama kupitia mikakati madhubuti inayowezesha maendeleo endelevu. Alibainisha kuwa LVRLAC ina kanda tatu – Tanzania, Kenya na Uganda – na kwamba Tanzania inaongoza kwa mafanikio.
Aidha, moja ya ajenda muhimu zilizojadiliwa ni namna ya kutatua changamoto ya magugu maji katika eneo la Busisi–Sengerema, kama sehemu ya majukumu ya LVRLAC ya kulinda usafi wa Ziwa Victoria.
Awali Mhe. Dkt. Dugange alizindua kampeni ya kuhimiza Matumizi ya Nishati Safi ya kupikia pamoja na kugawa majiko kwa Baba lishe na Mama lishe. Kampeni hiyo inaendeshwa na Mtandao wa Wanawake Viongozi wa LVRLAC.
Barabara ya Balewa
Sanduku la Posta: 1333,Mwanza
Simu: +255 28 250 1375
Simu ya Kiganjani: 0755741738
Barua Pepe: cd@mwanzacc.go.tz
Copyright ©2017 Mwanza City Council . All rights reserved.